Siku ya Kimataifa ya Watoto na Changamoto za Ugaidi na Fikra Potofu

Imehaririwa na Dkt., Ahmed Khalaf Abulfadl

  • | Thursday, 21 November, 2024
Siku ya Kimataifa ya Watoto na Changamoto za Ugaidi na Fikra Potofu

     Dunia huadhimisha Novemba 20 kila mwaka kama Siku ya Kimataifa ya Mtoto, siku iliyoanzishwa na Umoja wa Mataifa mwaka 1954 ili kuboresha ustawi wa watoto duniani na kuhakikisha mazingira salama kwa ajili ya ukuaji wao wa kihisia na kimwili. Siku hii ina umuhimu mkubwa kwa kuwa inaajmbatana na kupitishwa kwa Mkataba wa Haki za Mtoto mwaka 1989, ambao ni moja ya nyaraka muhimu zaidi katika kulinda haki za watoto na kuwalinda dhidi ya unyanyasaji na ubaguzi.

Ugaidi na Itikadi Kali: Tishio kwa Utoto

Katika miaka ya hivi karibuni, tishio la ugaidi na itikadi kali limeongezeka, likiwaathiri watoto moja kwa moja na kwa njia zisizo za moja kwa moja. Athari hizi zinajidhihirisha kwa njia kadhaa:

  1. Utekwaji wa Watoto kwa Nguvu

Maelfu ya watoto katika maeneo yenye migogoro wanatekwa kwa nguvu na makundi ya kigaidi kama vile Boko Haram na Al-Shabaab. Wanageuzwa kuwa askari wa watoto au washambuliaji wa kujitoa mhanga, jambo linalowaharibia utoto wao. Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) ya mwaka 2023, zaidi ya watoto 8,000 barani Afrika walihusishwa na makundi yenye silaha.

  1. Madhara ya Kisaikolojia na Kijamii

Watoto wanaoishi katika maeneo yenye migogoro hukumbwa na hofu isiyokoma ya mashambulizi ya kigaidi, hali inayosababisha matatizo ya muda mrefu ya kisaikolojia kama vile sonona na msongo wa mawazo wa muda mrefu (PTSD). Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins mwaka 2022 ulionyesha kuwa asilimia 60 ya watoto waliokulia katika maeneo yenye vita wana matatizo makubwa ya kisaikolojia yanayoathiri masomo yao na uwezo wa kuunda mahusiano ya kawaida.

  1. Kunyongewa Elimu

Ugaidi huathiri moja kwa moja miundombinu ya elimu, ambapo shule zinashambuliwa au kutumiwa kama kambi za kijeshi. Kwa mfano, UNICEF iliripoti kuwa takribani watoto milioni 222 duniani walinyimwa fursa ya kupata elimu kwa sababu ya migogoro ya silaha, hali inayoongeza uwezekano wao wa kujiunga na itikadi kali.

  1. Watoto Kama Wahanga wa Moja kwa Moja

Watoto mara nyingi wanakuwa malengo rahisi ya ugaidi. Mashambulizi kwenye shule, kama lile la Shule ya Peshawar huko Pakistan mwaka 2014 lililoua watoto 132, yanaonyesha jinsi makundi ya kigaidi yanavyotumia ukatili wao dhidi ya watoto wasio na hatia.

Jukumu la Jumuiya ya Kimataifa katika Kuwalinda Watoto Dhidi ya Itikadi Kali

Ili kukabiliana na changamoto hii, jumuiya ya kimataifa inapaswa kushirikiana kwa nguvu katika maeneo yafuatayo:

  1. Kuimarisha Elimu

Elimu ni silaha bora zaidi ya kupambana na ugaidi na itikadi kali. Kupitia mazingira salama ya kielimu na mitaala inayokuza maadili ya kibinadamu na uvumilivu, tunaweza kupunguza hatari ya watoto kushawishiwa na makundi yenye itikadi kali.

  1. Kuwekeza katika Programu za Urejesho

Kuna umuhimu mkubwa wa kuanzisha programu maalum za kuwasaidia watoto waliopona kutoka kwa makundi ya kigaidi, ili kuwaondoa katika fikra za itikadi kali na kuwasaidia kujiunga tena na jamii.

  1. Kuimarisha Mikataba ya Kimataifa

Serikali zinapaswa kuhakikisha utekelezaji kamili wa Mkataba wa Haki za Mtoto na viambatisho vyake, ambavyo vinataka watoto walindwe dhidi ya unyonyaji katika migogoro ya silaha.

  1. Kuongeza Uelewa wa Kijamii

Kuelimisha jamii juu ya madhara ya ugaidi na itikadi kali kwa watoto inapaswa kuwa sehemu ya mipango ya kitaifa na kimataifa. Kampeni za vyombo vya habari na elimu zinaweza kusaidia kuwalinda watoto dhidi ya propaganda za itikadi kali.

Hitimisho

Siku ya Kimataifa ya Mtoto si tu tukio la kusherehekea, bali ni mwito wa kutafakari na kuchukua hatua za kuboresha hali ya watoto duniani. Kulinda watoto dhidi ya hatari za ugaidi na itikadi kali si jukumu la serikali pekee, bali ni wajibu wa pamoja unaohitaji mshikamano wa kimataifa na wa kitaifa. Kama alivyosema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika ripoti yake ya mwaka 2022: “Watoto ni matumaini ya siku zijazo, na kuwaokoa kutoka kwenye giza la ugaidi na itikadi kali ni uwekezaji katika mustakabali wa binadamu wote.”

Print
Categories: Makala
Tags:
Rate this article:
No rating

Please login or register to post comments.